Alhamisi, 28 Mei 2015

SHUKRANI YA PONDA

Ilikuwa ni kazi ambayo nilijua kabisa rafiki yangu Joyce angeweza kuifanya, moja kwa moja nilimpigia simu na kumjulisha ili aweze kupeleka vyeti vyake. Ni muda mrefu Joyce alikuwa akihangaika huku na kule kutafuta ajira hivyo niliamua kumsaidia ili aweze kufanikiwa kupata kazi. Baada ya kumueleza Joyce alifurahi sana na haraka alikwenda kupeleka vyeti vyake na baadaye alifanyiwa usaili, na baada ya wiki mbili tu alifanikiwa kupata kazi katika kampuni ya Sigara. Maisha yaliendelea na sasa wote tulikuwa na kazi. Siku moja nikiwa nyumbani nimepumzika Joyce alifika huku akionekana kuwa mwenye furaha sana "Mary rafiki yangu, sasa mambo yangu ni mazuri, yaani hapa nilipo ninafuraha sana, yaani hata sijui nianzie wapi kukueleza".
Nilimtizama huku nikionyesha tabasamu zito nikiwa na shauku kubwa la kutaka kujua kwanini Joyce alikuwa amefurahi kiasi kile "Ehee niambie rafiki kuna nini tena" Aliguna kidogo kisha akasogea na kuketi karibu yangu huku akinionyesha karatasi ambayo ilikuwa na maandishi ambayo nilishindwa kuyasoma kwa haraka kwasababu Joyce alikuwa akihangaisha mikono yake bila kutulia, "Yaani Mary mwenzio naenda Marekani umeona hii barua ni kwamba kuna nafasi za kazi, zimetoka hivyo na mimi nimejaza fomu na hivyo nimechaguliwa kwaajili ya kwenda kusoma na kufanya kazi, hapa nilipo ninafuraha isiyo na kifani".
Nilifurahi sana kusikia rafiki yangu kipenzi ndoto zake zinakamilika "Hongera sana (my dear)mpendwa, Mungu akutangulie, katika kila jambo hiyo ni hatua kubwa sana, sasa mbona hukuniambia na mimi mapema ningejaribu bahati yangu?" Joyce alicheka na kusema "Unajua hizi nafasi zilikuwa chache na maalumu kwa wafanyakazi wa kampuni ninayofanyia kazi hivyo hata ningekuambia usingeweza kufanikiwa" Tulizungumza sana siku hiyo na nilimtakia kila la heri baadaye aliondoka.

SIMULIZI FUPI YA KIFAMILIA

“Nilipofika nyumbani usiku ule, mke wangu
aliponitayarishia chakula, nilimshika mkono na
kumwambia, Kuna kitu nataka nikwambie. Mke
wangu alikaa chini na kula chakula kimya akiwa
tayari kunisikiliza. Tena nikagundua macho yake
yalionyesha anaumizwa. Nilishindwa hata namna
ya kuanza kufumbua kinywa changu. Lakini ilibidi
nimwam
bie ili ajue nilikuwa nikifikiri nini juu yake.
Nataka kukupa talaka. Nilianza kusema kwa
utulivu. Alionekana kutokereka na maneno yangu
badala yake aliniuliza kwa sauti ya upole ‘kwa
nini?’ Sikumjibu swali lake. Kutojibu kulimfanya
akasirike. Akatupa kijiko na akanikaripia, ‘wewe si
mwanamume!’ Usiku ule, hakukuwa na maongezi
kati yetu. Alikuwa akilia kwa kwikwi. Nilifahamu
kwamba alitaka kujua ni nini kimetokea kwenye
ndoa yetu. Lakini kwa hakika nisingeweza kumpa
jibu wala sababu ya kuridhisha; alionekana si mali
kitu kwangu penzi langu lilihamia kwa Mary.
Sikumpenda tena mke wangu mawazo yote
yalikuwa kwa Mary. Kwa kweli nilimdharau mke
wangu!

NILIMTAFUTA MIAKA SITA


  Nakumbuka ilikuwa ni siku ya alhamisi nilipokutana naye kwa mara ya kwanza.Siku hiyo nilikuwa shuleni,alipokuja shuleni kwetu.
Nilikuwa nje nikimalizia muda wa mapumziko,niliegemea kwenye nguzo ya nje ya darasa letu,nimeinama nikiwaza juu ya ombi la John la kuwa naye kimahusiano ya kimapenzi aliloniambia jana.
            Nilipoinua kichwa changu nilimwona mvulana mgeni katika macho yangu, mrefu na mwenye mwili mwembamba,alikuwa amependeza sana.Si kwamba alivaa vipi ,ni jinsi ya rangi ya bluu na fulana nyekundu,ndiyo iliyomfanya aonekane simati na kunitoa udenda.
Alipozidi kusogea karibu na kuonekana barabara  mapigo ya moyo yalibadilika nikaona yanaanza kwenda mbio mbio.Mfumo wangu wa damu ulibadilika,damu ikaanza kwenda kwa kasi zaidi.
Ni upendo mkubwa uliojitokeza baada ya kuonana na Krisi,moyo wangu ulivutiwa sana na mwonekano wake tu,ingawa sikuwa namfahamu tabia yake na hata jina ,sikulifahamu ,lakini hayo yote hayakuwa na nafasi katika fikra zangu.

NISAMEHE EID MUBARAK

LABDA haitakuwa sahihi nikilalamika sana maana sina wa kumlaumu.
Haitakuwa na maana nikilia sana huenda chozi langu linazidi kumkera mwenyezi Mungu muumba mbingu na nchi.
Natamani sana kumwomba mungu msamaha lakini si sawa kama sitatubu katika dunia kwanza!!
Ewe mwenye moyo nisikilize kwa makini, nakuandikia haya katika sikukuu ya Iddi maana nayakumbuka machungu mengi sana, si machungu ya kuletewa na mtu bali kwa uzembe wangu mwenyewe. Uzem,be wa kuchanganua mambo na kujua zipi pumba na upi mchele.
Nipe sikio na moyo wako sasa, maana mimi ni mfano kwenu. Mfano mbaya usiofaa kuigwa bali kuwafunzi watoto wenu na vizazi vijavyo. Yawezekana pia mimi ni mfano kwako wewe ili kama hujaingia shimoni usiingie kamwe!!!
MNAMO miaka mitatu iliyopita, nikiwa nimemaliza shahada yangu ya kwanza ya ualimu. Nilibahatika kukutana na msichana ambaye sijui nimwelezee vipi ili utambue kuwa alinivutia.
Tabia zake tangu aliponipisha kiti niketi ndani ya daladala baada tu ya kutambua kuwa mimi ni mrefu sana hivyo naumia sana kuinama katika daladala ile.
Msichana wa mjini kumpisha kiti kijana mwenzake ndani ya daladala? Ilinistaajabisha.
Ningekosa ustaarabu iwapo nisingetoa shukrani kwa mwanadada yule, na hapo ukaribu wetu ukaanzia. Akanipa namba yake ya simu bila kusita. Akanieleza kuwa anakaa Gongo La mboto nami nikamweleza kuwa ni mwenyeji wa Dar lakini nipo Mombasa kikazi na nd’o kwanza nimepata ajira.
Bahati nzuri aliwahi kufika Mombasa pia, hilo jambo likatuweka karibu zaidi.
Hata nilipofika nyumbani na kuwasimulia watu wakanieleza kuwa huenda ni bahati yangu na huyo ni mke ameletwa katika namna ya maajabu.

ABUNUASI NA HUKUMU YA KIJANA.


Hapo zamani za kale katika nchi moja Afrika, paliishi mama mmoja ambaye alikuwa mjane. Muda mfupi tu kabla ya mumewe kufariki walijaliwa mtoto mmoja wa kiume ambaye huyo mama alimlea kwa shida na taabu nyingi. Hata hivyo mama na mtoto wake walipendana ipasavyo. Hapo katika kijiji chao kulikuwa pia na tajiri mmoja ambaye alikuwa bahili na katili kweli. Yule kijana maskini alikwenda kwa tajiri kuomba kazi. Tajiri alimwambia kwamba alikuwa na kazi kwake na angemlipa vizuri sana.
Kijana alifurahi kusikia hivyo na akamwuliza tajiri kwa furaha.
"Kazi gani hiyo utanipa mheshimiwa? Mimi nitaifanya vizuri mpaka hata wewe utafurahia."
Tajiri akamwambia, "Ukilala katika maji baridi sana usiku mzima, nitakupa shillingi laki moja." Ulikuwa wakati wa baridi sana kwamba maji ya ziwa karibu yagandamane kuwa theluji kwa baridi.
Lo! Kijana hakufikiria angeweza kuwa na pesa nyingi hivyo katika maisha yake. Tamaa ya kutaka kumsaidia mama yake ambaye wakati huo alikuwa mgonjwa na mzee, ilikuwa kubwa sana kwa hivyo akakubali bila kufikiria. Mama aliposikia habari hizo karibu azimie kwa wasiwasi na huzuni.
"Mwanangu sitaki uhatarishe maisha yako kwa sababu ya pesa. Mungu yuko nasi na hajatuacha hata siku moja tukalala njaa. Atazidi kufanya hivyo hivyo. Je, ukifa nitabaki na nani mwanangu? Mimi mzee sasa wala sijiwezi!" Kijana alimjibu,
"Mama usiwe na wasiwasi wala woga wo wote! Nitaweza kabisa kulala kwenye maji baridi mpaka asubuhi na siwezi kufa" Mama bado alizidi kubisha, lakini kijana alisisitiza kabisa kwamba lazima afanye hiyo kazi ambayo itawaondolea shida zote za kifedha, kama alivyoona yeye.

Jumatano, 27 Mei 2015

HATAKAMA UKIANDAMWANA NA MATATIZO,MAJARIBU USIABUDU MIUNGU MINGINE

Mama mmoja baada ya kukaa kwa muda mrefu bila kushika mimba, aliamua kwenda kwa mchungaji mmoja ambaye alitoka nchi ya mbali na kuja pale mtaani kwao akiwafanyia watu miujiza mbalimbali kupitia maombi yake na mama akaomba kuombewa ili apate mtoto.

Mchungaji yule alimfanyia ibada fupi na miezi michache baadae yule mama alibahatika kupata mimba na kuibeba kwa miezi tisa kisha akajifungua salama mtoto wa kiume.

Mama yule aliendelea kumtunza mwanae kwa kumnyonyesha ingawa kila alipomnyonyesha mtoto yule mama aliishiwa nguvu na kulala kwa muda kabla ya kuamka na kuendelea na kazi.

Jambo lile lilimshtua sana mama lakini akafikiri labda ni tatizo la kawaida kwani hakuwahi kuwa na mtoto.

Akaamua amwanzishie kumpa maziwa na kumwomba msichana wake wa kazi kuwa awe anampa maziwa pindi yeye yupo kazini na akawa akinunua maziwa lita tatu ili yaweze kukaa kwa siku tatu.

Maajabu ni kwamba lita tatu ziliisha kwa siku na mama kwa kuwa alipenda kwenda na bajeti hivyo alimkaripia msichana wa kazi na kumpiga sana kwa kumaliza maziwa lita tatu kwa siku.

Binti alilalamika sana na kusema mama huwa nayachemsha na kuyaacha mengine kwenye sufuria kisha kidogo namnywesha mtoto na ninaendelea na kazi kabla ya kuja kuangalia na kuona mazima yameisha kwenye sufuria.

Mama hakuamini na binti akaamua kuweka mtego ili aone kama ni majirani wanamfanyia visa au kuna kitu ambacho hunywa maziwa yale.

Jumanne, 26 Mei 2015

“ASANTE MAMA WA KAMBO!!”

SHAMRA shamra zilizidi kurindima kwa fujo katika ukumbi wa Sabasaba wilayani Temeke, hakika maharusi walikuwa wamependeza na utakuwa mchoyo wa kuzaliwa usingewapongeza waliotumia ubunifu wa hali ya juu kuupamba ukumbi ule nao ukapambika.
Kila mmoja alitabasamu bila kujalisha linatoka moyoni ama ni la kuzugia!!
Wanawake walipiga vigelegele na wanaume walipiga mbinja kila muda ambapo msema chochote aliamuru!!
Naam!! Ilikuwa sherehe ya aina yake ya kuwaunganisha Maria na Christian kuwa mwili mmoja!!!
Chris alikuwa mwenye furaha sana alipopewa nafasai ya kusema chochote, alizishukuru pande mbili akianza na ule upande wa ukweni akawashukuru kwa zawadi ya mke mwema…..kisha akageukia upande wa pili na kuwashukuru wazazi wake waliomkuza na kumpa elimu dunia pamoja na ile ya darasani!!!
Hatimaye msema chochote akamkabidhi kipaza sauti Maria!!
Ukumbi mzima ulitambua kuwa Maria hakuwa akitabasamu kutoka moyoni lakini bado hakuna aliyejua kwanini alikuwa katika hali ile.
Maria akashika kipaza sauti mbele ya umati na kuanza kuzungumza.
“Imekuwa safari ndefu sana hadi kuifikia siku hii ya leo…nikimtoa mwenyezi Mungu katika safari hii ninaye mtu mwingine muhimu katika dunia hii wa kumshukuru!! Ni mtu mmoja tu nasisitiza pasipokuwa na unafiki wowote!!
Namshukuru mama yangu…mama yangu wa Kambo” akasita kidogo ukumbi nao ukawa kimya!! Kimya kikuu…Maria akaendelea.

Jumatano, 20 Mei 2015

STORI YA “NITAKUBEBA KILA ASUBUHI MKE WANGU MPAKA KIFO KITAKAPO TUTENGANISHA”









“Nilipofika nyumbani usiku ule, mke wangu aliponitayarishia chakula, nilimshika mkono na kumwambia, Kuna kitu nataka nikwambie. Mke wangu alikaa chini na kula chakula kimya akiwa tayari kunisikiliza. Tena nikagundua macho yake yalionyesha anaumizwa. Nilishindwa hata namna ya kuanza kufumbua kinywa changu.
Lakini ilibidi nimwambie ili ajue nilikuwa nikifikiri nini juu yake.Nataka kukupa talaka. Nilianza kusema kwa utulivu . Alionekana kutokereka na maneno yangu badala yake aliniuliza kwa sauti ya upole ‘kwa nini ?’ Sikumjibu swali lake. Kutojibu kulimfanya akasirike . Akatupa kijiko na akanikaripia , ‘wewe si mwanamume!’ Usiku ule, hakukuwa na maongezi kati yetu. Alikuwa akilia kwa kwikwi. Nilifahamu kwamba alitaka kujua ni nini kimetokea kwenye ndoa yetu . Lakini kwa hakika nisingeweza kumpa jibu wala sababu ya kuridhisha; alionekana si mali kitu kwangu penzi langu lilihamia kwa Husna. Sikumpenda tena mke wangu mawazo yote yalikuwa kwa Husna. Kwa kweli nilimdharau mke wangu !Huku moyo wangu ukijua wazi kwamba nafanya kosa , niliandika talaka ambayo ilionyesha kwamba yeye (mke wangu) angepata nyumba yetu, gari na atakuwa na hisa 30% ya kampuni yetu. Aliangalia talaka ile na kuichana vipande vipande.Mke ambaye tumeishi nami kwa miaka 10 alionekana mgeni machoni mwangu .

MWANAUME MWENYE NGUVU KULIKO WOTE



 

UNAJUA jina la mwanamume mwenye nguvu kuliko wote? Ni mwamuzi Samsoni. Yehova anampa Samsoni nguvu hizo. Hata kabla ya Samsoni kuzaliwa, Yehova anamwambia mama yake hivi: ‘Upesi utazaa mwana. Ataongoza kuokoa Israeli kutokana na Wafilisti.’


Wafilisti ni watu wabaya wanaoishi Kanaani. Wana wanajeshi wengi, na wanawaumiza Waisraeli sana. Wakati mmoja, Samsoni anapokwenda kwa Wafilisti, simba mkubwa anatokea akinguruma kukutana naye. Lakini Samsoni anamwua simba huyo kwa mikono yake tu. Pia anaua mamia ya Wafilisti wabaya.
Baadaye Samsoni anapendana na mwanamke, Delila. Viongozi Wafilisti wanaahidi kwamba kila mmoja wao atampa Delila vipande 1,100 vya fedha akiwaambia kinachompa Samsoni nguvu nyingi hivyo. Delila anataka fedha zote hizo. Yeye si rafiki wa kweli wa Samsoni, wala wa watu wa Mungu. Anazidi kumwuliza Samsoni kinachompa nguvu nyingi hivyo.


Mwishowe, Delila amshawishi Samsoni. Naye Samsoni anamwambia siri ya nguvu zake, akisema: ‘Mimi sijanyolewa nywele. Tangu kuzaliwa kwangu, Mungu alinichagua niwe mtumishi wake wa pekee, yaani, Mnadhiri. Nikinyolewa nywele, nitapoteza nguvu.’

Jumanne, 19 Mei 2015

STORI YA KUSISIMUA NA KUSIKITISHA

nikiwa nimekaa leacture room
nikimuangalia msichana aliyekaribu
yangu,niliyekuwa nikimuita
"Bestfriend"nilikuwa nikimuangalia
nywele zake nzuri na sura yake ya
upole huku nikitamani awe
wangu,lakini yeye hakuwa
akitamani hilo na nilikuwa
nikilitambua hilo.
Baada ya leacture,alikuja kwangu
na kuniomba notes za siku ya
nyuma kwa sababu hakuweza
kuingia darasani hiyo siku

MAISHA NA MIKASA

Mwanzoni sikumpenda kutoka moyoni, nilimpenda kwa kuwa tu alikuwa mrembo haswa..kwa kifupi nilimtamani tu….yaani nilitegemea akinivulia nguo zake tukashiriki tendo hamu yangu itaisha na nitaachana naye. Ndio ningeachana naye kwa sababusikuona umuhimu wa kudumu na msichana ambaye sijui hata kama nitamuoa. Nilipomwambia tutaoana hakika nilidanganya Alinipenda sana, kadri siku zilivyokwenda alizidisha upendo wake kwangu. Hakuna nilichohitaji kwake akaninyima, aliwahi kumdanganya baba yake kuwa anaumwa akatumiwa pesa ilimradi anipatie mimi nilipomwambia kuwa kuna mtu ananidai na abananisumbua kwelikweli. Alisikitika kusikia vile, akaahidi kunipigania. Haikuwa kweli nilichomwambia juu ya kudaiwa, pesa ile aliyonipa niliitumia kulipia chumba nikafanya uzinzi na Fatuma. Alihadithiwa habari hiyo na marafiki walioniona nikiingia kule, akalia kwa uchungu mbele yangu, lakini neno lake la mwisho likabaki kuwa ‘NAKUPENDA SANA…..WEWE NI MWANAUME WA MAISHA YANGU’……..Nilij isikia vibaya lakini nafsi nyingine ikanikumbusha kuwa nilikuwa katika mahusiano na msichana yule kwa sababu moja tu…NGONO… na katu hakutaka kushiriki ngono na mimi. Alinikwepa sana hadi nikajisikia vibaya. Nikahisi huenda ana mtu mwingine. Hakika nilidhani kuwa anajihusisha na mtu mwingine ambaye hushiriki naye tendo hilo la ngono ambalo kwangu mimi kilikuwa kitu pekee ambacho kingeweza kuniaminisha kuwa ananipenda kweli. Msichana mrembo kama huyo kamwe asingeweza kuishi bila kufanya mapenzi. Hakika haikuniingia akilini. Wangapi wenye ,ali zao wanamtongoza, yeye ni nani hadi asiingie majaribuni?? Hapana ni uongo mtupu ananiongopea mimi. Nikaendelea na vimbwanga vya hapa na pale. Hakuchoka kunibembeleza, hakuchoka kunipenda na hakuchoka kunikumbusha kuwa ni mimi pekee nilikuwa katika moyo wake wa nyama. “Nikipotea jumla nd’o utajua kuwa nilikuwa nakupenda..” aliwahi kunambia neno hilo. Japo lilinigusa lakini sikulitilia maanani. Hatimaye tukamaliza shule, nikategemea kuwa ule muda wa kumfaidi msichana yule kingono ulikuwa umewadia. Lakini haikuwa hivyo, akaendelea kuwa mgumu huku akijitetea kwa sababu zisizokuwa na kichwa wala miguu. Mwanzoni nilidhani kuwa aliogopa kufanya mapenzi kabla hajamaliza shule, lakini ajabu hadi tulipomaliza bado alisimamia msimamo.

STORI FUPI YA KUHUZUNISHA NA YENYE MAFUNZO ASA KWA KINA DADA

 
 
 
 
 
"Nilipoingia katika mahusiano naye nilimuamini, nikampa kila kitu nilichoweza. Nakumbuka enzi zile nyumbani tulikuwa tuna ng’ombe, niliiba maziwa kila siku na kumpelekea kwao. Akanenepa!! Penzi letu likawa huru alipoanza maisha yake mwenyewe. Sikuwa najua lolote kuhusu mapenzi. Alinifundisha.

Nikaegemeza maisha yangu yote kwake. Akanifanya nikawa mtumwa wa ngono kila nikienda chumbani kwake. Kama haikutosha sasa akaanza kunifundisha kunywa pombe. Niliamini kuwa ndiye mume wangu mtarajiwa, kwa nini nikatae? Nilimkubalia kila kitu.

Alinilazimisha ngono hata nilipokuwa katika siku zangu. Kweli nilikuwa msomi na niliyajua madhara ya kufanya hivyo lakini sikutaka kumuudhi huyo niliyeamini kuwa ni mume wangu. Nilipenda tutumie kinga lakini aliipinga sana.
Nikapata mimba ya kwanza!! Hakuwa na pesa lakini alinilazimisha niitoe. Nikaiba pesa nyumbani nikafanyaalivyotaka. Kwa mara yakwanza nika toa mimba. Haikuniuma sana!! Niliamini kuwa ni yeye atakuja kunioa na atanifichia aibu hii.

Jumatatu, 18 Mei 2015

" SIJAPOTEZA FURAHA YANGU'



  Nilikuwa katika wakati mgumu sana, kwani hakuna aliyekuwa akinijali, lakini sikukata tamaa kwakuwa niliamini Mungu yupo pamoja nami. Kuna wakati nilijikuta nakata tamaa kutokana na watu wengi kunizungumzia maneno yasiyokuwa na ukweli wowote. Maisha yangu yalikuwa yamezungukwa na marafiki wengi ambao kwa kiasi kikubwa nilikuwa nikiwaonyesha upendo na kuwaamini kuwa ni watu wa muhimu sana katika maisha yangu, Lakini kumbe  haikuwa vile ninavyofikiria walikuwa wamejivika ngozi ya kondoo lakini mioyo yao ikiwa imejaa chuki juu yangu.
Katika Maeneo ya  Vijana Kinondoni jijini Dar es salaam  nilikuwa nikishi na  Mama yangu mkubwa, kwani sikubahatika kuishi na wazazi wangu Baba na Mama yangu walifariki nikiwa mdogo sana. Mama yangu mkubwa alinilea vizuri sana hadi nilipomaliza elimu yangu ya sekondari, na kufanikiwa kuanza  chuo cha uhasibu. Nikiwa chuoni nilikutana na marafiki mbalimbali.
 Saida alikuwa ni rafiki yangu kipenzi  pale chuoni. Siku moja nikiwa najisomea Saida alikuja na kusema "Rozi rafiki yangu, kuna jambo nataka kukuambia, lakini mwenzangu usije ukamwambia mtu yeyote kuwa mimi ndiye niliyekueleza jambo hili" Ilinibidi nishangae na kusema "Ni jambo gani hilo? Mbona unaniweka roho juu. "Maneno yameenea hapa chuoni, watu wanakusema sana vibaya, yaani sijui nianzie wapi kukueleza." Moyo wangu ulishtuka nikawa nimebaki nashangaa "He! Watu wananisema vibaya? Kwani mimi nimefanya nini? Mbona unanishangaza Saida embu kuwa muwazi uniambie ni kitu gani kinaendelea".

Saida aliguna kidogo nakusema "Rafiki yangu, hivi  ni kweli una uhusiano wa kimapenzi na mwalimu  wa hesabu. Mr Ngowi, ndiyo maana unafaulu vizuri somo lake?" Ilinibidi niweke daftari langu pembeni na kusema "Eti nini Saida, kina nani wanasema hivyo, jamani mbona watu wanapenda kuzungumza maneno ya uongo, mimi sina uhusiano wowote na mwalimu Ngowi" Saida akacheka nakusema "Basi watu wengi hapa chuo wanajua ni kweli na anayesambaza hayo maneno ni Lina, ila chonde chonde usije kunitaja" Nilijisikia vibaya sana siku hiyo kwani ukweli ni kwamba sikuwahi kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwalimu.

Siku zilivyozidi kwenda maneno yaliendelea na Saida alikuwa akija na kunieleza maneno ambayo yanzungumzwa kuhusu mimi. Nilivumia hali hiyo bila yakumuuliza mtu yeyote kwani nilikuwa sipendi ugomvi.Siku ya jumamosi na jumapili mara nyingi nilikuwa nikienda kushinda nyumbani. Ilikuwa ni jumamosi moja ambapo nilienda nyumbani na kumkuta mama yangu mkubwa akiwa amekasirika sana. Nilimsalimia lakini hakuniitikia jambo ambalo niliona siyo la kawaida.
 Nilijaribu kumsalimia tena ndipo aliponyanyuka na kunipiga kibao katika paji la uso wangu " Wewe mwendawazimu, mimi nakulipia ada, halafu unaenda kufanya mambo ya ajabu chuoni, hivi wewe ni mtu wa kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwalimu wako? Tena nimesikia  huwa haulali chuoni kila siku unakuja kuchukuliwa na wanaume tofauti, yaani unabadilisha wanaume kama nguo. Hivi hii tabia ya ukahaba umeipata wapi?" Nilibaki nimeduwaa huku nikmisema "Hapana Mama mimi sina tabia hiyo, siwezi kufanya hivyo, unanionea Mama" Nililia kwa uchungu kwani Mama aliendelea kunigombeza huku akinipiga makofi ya usoni bila ya kunisikiliza. 

Maisha yangu yalikosa furaha kwani kila kukicha yalikuwa yakiibuka mambo tofauti, lakini sikujua nani ambaye anaweza kunifanyia yote haya. Kwani moyoni mwangu nilikuwa najua sikuwahi kumkosea mtu yeyote.
 Baada ya wiki mbili huku nikiwa sina maelewano mazuri na familia yangu.Siku hiyo nilikuwa chumbani nimepumzika pale chuoni alikuja Lina huku akiwa na kikosi cha marafiki zake. "Tumechoshwa na maneno yako, Rozi wewe mwanamke ni mnafki sana, kwanini unapenda kutufuatilia maisha yetu, unanisema vibaya kwa watu kuwa mimi na uhusiano wa kimapenzi  na walimu, eti  ndiyo maana nafaulu vizuri, ukaona haitoshi ukaenda kumwambia mpenzi wangu mimi namsaliti. Kwanini unanifuatilia au unamtaka mpenzi wangu?". Aliongea Lina kwa sauti ya jazba.
 Nilinyanyuka pale kitandani na kuuliza "Mbona siwaelewi, Eti unasema mimi nakusema vibaya, hivii  unajua unanishangaza wewe Lina yaani wewe unavyonizungumzia mimi vibaya, unampelekea maneno ya uongo hadi Mama yangu mkubwa, umeona haitoshi unataka kunisingizia mimi nakusema vibaya." Baada ya mimi kusema hivyo wote walinyamaza kimya kwa muda huku wakitazamana, mmoja wao akauliza "Nani amekuambia hayo maneno, acha uongo Lina hajawahi kukusema vibaya" 

Kutokana na hasira nilizokuwa nazo kwa wakati huo niliamua kumtaja Saida, ndipo wote wakabaki wakishangaa kumbe Saida huyohuoyo ndiye aliyekuwa anawapelekea maneno kwamba mimi namzungumzia vibaya Lina. Kwa wakati huo Saida alikuwa hayupo tulimsubiri  hadi aliporudi na sasa kila mmoja alimvamia kwa maneno makali huku wakimwimbia kwa tabia yake mbaya ya kusema uongo na kuchonganisha watu. Nilijisikia vibaya sana kwani mtu niliyemuamini kama rafiki yangu ndiyo alikuwa na nia ya kunichonganisha na marafiki hadi familia yangu. Aliniomba msamaha, mwanzoni ilikuwa ni vigumu kumsamehe lakini baadaye niliamua kumsamehe na maisha yanaendelea SIJAPOTEZA FURAHA YANGU.

Kuwa makini, usiamini maneno yote unayoambiwa, na mtu yeyote yule ni vyema kuchunguza ili kuwa na uhakika wa kile ulichoambiwa vinginevyo unaweza kugombana na watu kwa jambo lisilokuwa na ukweli. wahenga wanasema KIKULACHO KI NGUONI MWAKO.

AKUFUKUZAYE AKUAMBII TOKA


 


"Mbona umepauka sana, au haujapaka mafuta, mmmh halafu unanenepa sana siku hizi" Nilimtizama Ashura na kusema "Mbona mimi najiona nipo kawaida na pia nimepaka mafuta." Huku akicheka kwa dharau Ashura aliingia ndani na kuniacha nikiwa nimesimama kibarazani. Nilijiuliza maswali mengi kwanini Ashura ananicheka nilijitizama huku nikihisi labda nina kasoro yoyote katika mwili wangu lakini sikuiona. Basi nilimpuuza na kuendelea na safari yangu.


Mimi ni mzaliwa wa Morogoro katika familia ya watoto watatu, Baada ya kumaliza kidato cha sita nilipata nafasi ya kuendelea na elimu ya chuo kikuu Dar es salaam, Kutokana na hali halisi ya maisha ya nyumbani nilipotokea wazazi wangu walikuwa hawana uwezo, hivyo ilinibidi nimuombe rafiki yangu Ashura anisaidie hifadhi katika chumba alichokuwa amepanga karibu na maeneo ya chuo. Ashura alinikubalia na hivyo nilipata sehemu ya kuishi bila ya kutumia gharama yoyote.

"USIMDHARAU MTU KUTOKANA NA KIPATO CHAKE"

 
Kuna vijana walikuwa wamekaa kijiweni huku wakizungumza, ghafla akapita kijana mmoja anaitwa Sudi na aliwasalimia, huku akiwa anaendelea na safari yake kwa bahati mbaya aliteleza na kuanguka, lakini hakuna hata kijana mmoja aliyenyanyuka na kumsaidia wote waliangua vicheko na mmoja wao akisema "Huyu jamaa atakufa kwa mawazo, si anaishi hapo mtaa wa pili kwa ndugu zake yaani hawana chochote ni masikini sana kazi yao ni kuombaomba" Huku wakiendelea kumcheka. 

Sudi alinyanyuka na kuendelea na safari bila ya kuzungumza chochote huku machozi yakionekana kumlengalenga aliwaza moyoni mwake "Watu wengi wananidharau kutokana na hali duni ya maisha niliyonayo, eeh Mungu nisaidie" Pale kijiweni waliendelea kuzungumza "Unajua umasikini ni mbaya sana, kwani siku zote ukiwa masikini, basi ujue utapata shida sana, na ukizingatia yule aliyenacho ndiyo anazidi kuwa nacho."

NI BORA KUKAA KIMYA.









Mara nyingi nilikuwa nikimshauri sana Sara, kuachana na mpenzi wake kutokana na mpenzi wake huyo kuwa na tabia mbaya. Ambapo wakati mwingine alikuwa akimpiga sana. Siku hiyo nilikuwa nyumbani nimepumzika ghafla nilisikia mlangoni kuna mtu anabisaha hodi kwa nguvu. "Suzi, Suzi, naomba ufungue mlango John ananiuwa" Ilikuwa ni sauti ya Sara nilinyanyuka haraka na kufungua mlango Sara alionekana kuumia  maeneo ya usoni nilishtuka sana kumuona katika hali ile "Hee! Umepatwa na nini Sara, mbona hivyo kulikoni?" Nilimuuuliza huku nikimkaribisha ndani.
 Aliingia na kuketi lakini bado alikuwa analia kwa uchungu huku akisema "Yaani mimi kweli John ni wakunifanyia hivi,  wakati nimemfumania na mwanamke mwingine? Halafu ananipiga" Nilisogea na kuketi karibu huku niki mliwaza "Pole sana Sara, lakini kwanini anakupiga, kwa kosa lipi ulilomfanyia, huyu mwanaume ana kichaa heee! na wewe rafiki yangu mwanaume kama huyo hakufai ni bora uachane naye kabisa. Embu tizama  umemfumania halafu anakupiga,  usiwe mjinga kiasi hicho Sara wanaume wapo wengi, kama yeye anakuona wa nini, basi ajue kuna wengine wanafikiria watakupata lini. Mwanaume gani mshamba huyo usipoangalia ipo siku atakuvunja mguu".

POMBE SI DAWA YA MAPENZI.

Jerome alikuwa na ndoto ya kuwa mfanyabiashara mkubwa sana, Alikuwa ni kijana mchapa kazi na wakati wote alikuwa makini sana. Katika maisha yake alisema kamwe hawezi kuchanganya kazi na mapenzi. Kijana huyu alikuwa ni mkarimu mtanashati na mwenye mvuto wa hali ya juu, baadhi ya wanawake walikuwa wakitamani kuwa karibu naye lakini Jerome alikuwa na msimamo hakutaka kabisa kujiingiza katika suala zima la mapenzi.

Akiwa anaendelea  kazi zake ambapo kazi zote alikuwa akizifanya akiwa anaishi Mkoa wa Dodoma. Baadaye alianza kusafiri  na kwenda katika mikoa mbalimbali hususani Mkoa wa Dar es salaam ambapo alikuwa akikutana na wafanyabiashara mbalimbali.


Siku moja akiwa jijini Dar es salaam katika shughuli zake alikutana na dada mmoja ambaye alikuwa ni mwanafunzi wa chuo na walifahamiana, na kisha kubadilishana namba za simu.

"SIWEZI KUKUACHA"



Nimechoka na kero za kila siku, sitaki kabisa yaani ni bora tu niondoke nirudi kwetu"  Stara Alikuwa anazungumza kwa sauti iliyoonyesha kuwa na uchungu sana kutokana na tabia za mume wake ambaye alikuwa anachelewa kurudi nyumbani na akirudi anakuwa amelewa sana. Hali hii ilikuwa inamuumiza sana Stara ambaye alikuwa anavumilia kwasababu alikuwa anampenda mume wake.

Maisha ya Stara na mume wake kabla ya kuingia kwenye ndoa yalikuwa ni maisha yaliyojaa furaha na upendo, lakini baada ya kuingia kwenye ndoa mambo yalibadilika, Kutokana na hali hiyo Stara alikuwa akiumia sana  ilifikia kipindi akawa anashindwa kuvumilia kutokana na tabia ya mume wake kumpiga,  na kuna wakati alikuwa akirudi amelewa usiku wa manane alikuwa akimlazimisha  Stara kuwa naye kimepenzi kwa nguvu hata kama Stara akisema anaumwa, yeye alifanya nguvu yaani alikuwa akimbaka mke wake kutokana na kumtaka kimapenzi kwa nguvu bila ya kumuandaa. Stara aliumia sana.

"WIFI NIMEKUCHOKA"

Katika maisha unaambiwa mvumilivu hula mbivu, kwani siku zote hakuna safari ya maisha isiyokukuwa na changamoto,Monalisa aliolewa na Jerome na kufanikiwa kupata watoto wawili walikuwa wakiishi katika nyumba ya kupanga na kutokana na hali ya maisha walikuwa wamepanga vyumba viwili, Watoto walikuwa wakilala sebuleni.Wakiwa wanaendelea kuishi huku wakihangaika kutafuta pesa ya kujikimu katika maisha, Siku moja wakiwa nyumbani majira ya saa moja jioni walisikia mlango ukibishwa hodi.

 Monalisa alinyanyuka na kufungua mlango kumbe alikuwa amekuja wifi yake ambaye alikuwa ambeba begi lake kubwa na mfuko wa Rambo, Alimkaribisha ndani na kumsaidia kubeba begi. Wifi huyu alikuwa ametokea Kijijini  Morogoro na alifika kwa kaka yake ili aweze kutafutiwa shule, Basi alikaribishwa  vizuri bila matatizo yoyote, Kutokana na nyumba kuwa ndogo ilimbidi ajumuike kulala pamoja na watoto pale sebuleni ambapo walikuwa wakitandika godoro na kulala pamoja. Maisha yaliendelea, huku wifi akiwa anaishi pale nyumbani, siku zote alikuwa akiamka asubuhi lakini asimsaidie Monalisa kufanya kazi yoyote.


Hivyo Monalisa alikuwa akimka mapema nakuandaa kifungua kinywa na wakati mwingine ilimbidi apike chakula asubuhi kwaajili ya kuwaachia watoto halafu ndiyo aondoke kwenda kwenye biashara yake ya kuuza samaki.Maisha yaliendelea hivyo hivyo ndipo sikumoja Monalisa aliamua kumueleza mume wake tabia za mdogo wake kukaa bila ya kufanya kazi yoyote na ukizingatia alikuwa ni msichana mkubwa, Jerome alijaribu kumwelekeza mdogo wake bila mafanikio kwani sasa ndiyo alileta mtafaruku zaidi kati ya Monalisa na wifi yake, sasa Wifi alianza kununa bila sababu na kumchukia sana wifi yake. 

Hali ile ilikuwa inamuumiza sana Monalisa ambaye alikuwa akihangaika siku zote ili nyumbani watoto waweze kupata chakula, na Mume wake alikuwa ni fundi seremala, na hata alipokuwa akipata pesa mara zote alikuwa akimpa mdogo wake kwahiyo ilimbidi Monalisa, ajibane sana katika kutafuta pesa kwaajili ya matumizi ya pale nyumbani. Baada ya miezi sita kupita wifi yake Monalisa vituko ndiyo vilizidi sasa alianza kuleta wanaume pale nyumbani. Siku zote alikuwa akisubiri watoto wakiwa wameenda shule, na Baba na Mama wakiwa wameenda kazini, na kutumia muda huo kuingiza wanaume, na huku akitumia kitanda cha kaka yake bila ya kujali chochote, tabia hiyo iliendelea hadi siku ambay
o Monalisa aligundua kuwa shuka lilikuwa limechafuka na kumuuliza wifi yake ambaye alikasirika sana.

 Huku akiwasingizia watoto walikuwa wakicheza kitandani, lakini watoto walikanusha huku wakilia kuwa wamesingiziwa. Baadaye Monalisa alipuuzia lakini wifi yake hakuacha hiyo tabia, ndipo siku moja jirani aliamua kumueleza Monalisa kile kinachoendelea akiwa hayupo.Monalisa alisikitika sana na sasa aliwaza namna ya kumfumania wifi yake. 

Siku hiyo alikwenda kazini kama kawaida lakini hakukaa muda mrefu akawa anawasiliana na yule jirani ambaye alimwambia kuwa muda huo kuna mwanaume amefika pale nyumbani. Moja kwa moja Monalisa aliondoka kijiweni na kurudi nyumbani ambapo alimkuta wifi yake akiwa amejipumzisha kitandani kwake na mwanaume huku wakifanya starehe zao, Alishtuka sana na kuanza kumfokea huku akimtaka aondoke."Wifi nimekuchoka, naomba uondoke, aibu gani hii jamani, unawafundisha nini watoto wangu naomba uondoke sitaki kukuona kabisa"

 Wifi kwa hofu alianza kulia na kuomba msamaha kwa Monalisa asimueleze kaka yake.Lakini Monalisa alimuambia haiwezekani amekwisha mvumilia vya kutosha lazima aondoke, Baadaye Jerome aliporudi kutoka kazini Monalisa alimweleza kila kitu ndipo kaka mtu alipoamua kumrudisha mdogo wake kijijini kwa kuchoshwa na tabia za mdogo wake.Wifi aliomba msamaha, na Monalisa alimsamehe lakini alimwambia ni vyema angerudi nyumbani Morogoro.

"WIFI MTATA"










Alipomaliza chuo tu Justa aliolewa na Mfaume kijana huyu alikuwa ni mfanyabiashara,  ambaye alikuwa akimpenda sana Justa. Mfaume alikuwa akiishi na mdogo wake wa kike aliyekuwa anaitwa Leti kwa kipindi hicho Leti alikuwa bado anasoma chuo. Baada ya Justa kuolewa sasa alihamia na kuishi pamoja na mume na wifi yake, maisha yalikuwa mazuri kwani Mfaume alikuwa anampenda sana mke wake. Kwa kipindi hicho Justa alikuwa bado hajafanikiwa kupata kazi hivyo alikuwa ni Mama wa nyumbani huku akiwa anaendelea kutafuta kazi. 
Siku zote Mfaume alikuwa akiacha pesa za matumizi pale nyumbani na  alikuwa akimpa mdogo wake pesa hizo yaani hata pale mke wake alipokuwa na shida ilimbidi amweleze wifi yake kwani mume wake alikuwa akimpatia pesa zote za matumizi ya pale nyumbani mdogo wake.Hali ile ilikuwa inamuumza sana Justa na ndipo alipoamua kumwambia mume wake kuwa hapendezewi na tabia yake  lakini mwanaume huyo hakutaka kumsikiliza.

"....NDUGU LAWAMA....."

 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
"Asante sana shemeji Beni kwa msaada ulionipa, lakini nilikuwa naomba uniongezee kiasi cha shilingi laki tano tu, kuna jambo nataka kulifanya, nimepungukiwa kidogo, naimani utanisaidia". Alikuwa ni shemeji yangu ambaye ni kwa kipindi kirefu nimekuwa nikimsaidia kuendeleza biashara zake,  kwa wakati huo nilikuwa sina kiasi  hicho cha fedha "Ningependa kukusaidia shemeji lakini hali yangu kiuchumi kwa sasa imeyumba ila usiwe na shaka nitafanya mikakati ndani ya siku mbili tatu nitakupa hiyo pesa.lakini shemeji kuwa makini sana na utumiaji  wa pesa kwani kwa sasa pesa imekuwa ngumu kupatikana hivyo ni vyema ukawa makini sana katika biashara yako". Baada ya kumaliza mazungumzo shemeji alinielewa na kuondoka.

Kesho yake asubuhi ilikuwa ni siku ya jumamosi ambapo siku hiyo si kwenda kazini, alikuja dada yangu akiwa pamoja na mtoto wake mdogo wa kike.  "Habari za masiku dada, karibu sana" Dada alinitizama huku akisema "Kaka habari yangu si njema kwani hapa nilipo, nimekuja kwako nina shida  mtoto amerudishwa nyumbani kwasababu ya anadaiwa ada, sasa kaka naomba unisaidie shilingi laki tatu niweze kumrudisha  mjomba wako shule, yaani hapa nilipo sina mtu mwingine wa kumtegemea zaidi yako". 
Nilikuwa nimeketi  pale sebuleni huku nikiwaza na nafsi yangu "Mhhh hapa nilipo leo nimeamka nina shilingi elfu kumi na tano tu mfukoni mwangu sasa nitawezaje kumsaidia dada yangu" Nilimtizama dada na kusema "Daah, hali ni mbaya sana dada yangu, umenikuta sina pesa kabisa lakini embu subiri naweza kumkopa rafiki yangu kiasi hicho cha pesa ili mtoto aende shule." Nilimpigia simu rafiki yangu anaitwa Zuberi na kumuomba anikopeshe pesa kidogo, kwa bahati nzuri nilifanikiwa hivyo nilimpa kiasi kile cha fedha dada.

Baada ya dada yangu kuondoka mke wangu alikuja  akiwa ametoka sokoni "Mume wangu imekuwa ni vizuri nimekukuta kwani mama amenipigia simu alikuwa anataka kuongea na wewe" Basi moja kwa moja mke wangu akampigia simu Mama mkwe wangu  kisha akanipa simu niongee naye. "Shikamoo Mama habari za hapo nyumbani" Mama aliitika kwa sauti ya unyonge "Habari si njema mwanangu  mwili unaniuma sana, halafu sina pesa kabisa, naomba unitumie hela ya kununua mchele na sukari pamoja na ya kwenda Hospitali" Nilikuwa nikimsikiliza kwa umakini na baadaye nilimuahidi kuwa nitamtumia pesa kwaajili ya matibabu na chakula. Nilikuwa sina hela ilinibidi nikope pesa kwaajili ya kumtumia mama mkwe.

Baada  ya siku tatu kupita yule shemeji yangu alinipigia simu na kunikumbusha kile kiasi cha pesa alichoniomba, kwa bahati nzuri siku hiyo nilikuwa nimefanikiwa kupata pesa katika biashara zangu hivyo sikusita kumsaidia. Maisha yangu yalikuwa yamezungukwa ndugu wengi waliokuwa wakinitegemea katika mahitaji mbalimbali ijapokuwa nilikuwa sina uwezo mkubwa sana kifedha. Lakini nilijitahidi kwa kila hali kuhakikisha nawasaidia.
Baada ya miaka mitatu siku moja nikiwa natoka kazini nilipata ajali nikiwa naendesha gari aina ya Corola, na kunisababishia kuvunjika miguu, nilikuwa katika wakati mgumu sana kwani nilikuwa sina uwezo wa kufanya kazi tena.
 Na sasa nilikuwa nahitaji msaada kwa ndugu zangu, lakini chakushangaza wale ndugu niliokuwa nawasaidia hata sikumoja hakuna aliyekuja kunisaidia kwa chochote, walikuja kunisalimia maramoja tu na baada ya hapo sikumuona tena ndugu yeyote. Siku moja alikuja shemeji yangu na Mama mkwe  kwa nia ya kumshauri mke wangu aniache kwani sina uwezo wa kumsaidia. Niliumia sana moyoni "Inamaana leo hii  mimi Beni, naonekana sifai baada ya kupata ajali, na mbona nilikuwa nikiwasaidia sana, hivi ni kweli wananichukia kiasi hiki. Mungu nisaidie nipone, ama kweli binadamu  hawatabiriki."

Mke wangu, alikuwa na msimamo na hivyo hakuniacha aliendelea kuwa na mimi hivyohivyo. Ndugu zake walimtenga kabisa, kwasababu yangu.Maisha yalliendelea  baada ya mwaka mmoja kupita, hatimaye nilipona kabisa nakurudi katika hali yangu ya kawaida. Nilirudi katika kazi yangu ya awali  bila matatizo. Kwani nilipokelewa vizuri na sasa nilipandishwa cheo. Maisha yangu yalirudi katika ramani nzuri, wale ndugu walionikimbia wakati naumwa, baada ya kusikia kuwa nimerudi kazini. haikuchukua muda walianza kuja kunitembelea tena wakijidai wamekuja kunijulia hali.Lakini kwasababu tayari nilikuwa nimejifunza mambo mengi hivyo nilijua namna gani naweza kuishi nao. Safari hii nilikuwa makini zaidi. Sikutaka kulipiza kisasi  naishi nao vizuri. 

AMA KWELI BINADAMU HAWATABIRIKI, ANAWEZA KUKUPENDA UKIWA NACHO UKIWA HAUNA KITU ANAKUKIMBIA.

TAMAA IMENIPONZA


                                              Ritha alikuwa ni msichana mrembo sana,  kila aliyemtizama alivutiwa na urembo alionao, na hata yeye alijitambua kuwa ni mrembo. Katika maisha yake Ritha  alikuwa anapenda sana vitu vizuri na vinavyokwenda na wakati kama nguo, viatu, simu na vitu vingine kadha kwa kadha. Lakini wazazi wake walikuwa hawana uwezo wa kumnunulia vitu vyote hivyo.

 Baada ya kumaliza  kidato cha nne, kwa bahati mbaya hakufanikiwa kuendelea na kidato cha sita na hivyo wazazi wake waliamua kumtafutia chuo.Akiwa  anasoma chuo alikutana na marafiki wa aina mbalimbali na marafiki zake wakubwa walikuwa ni wale ambao wametokea katika familia  ambazo wanajiweza yaani matajiri. Kutokana na wazazi wao kuwa na pesa walikuwa wakimiliki simu nzuri, na kompyuta (laptop) lakini kwa upande wa Ritha alikuwa hana hata simu ya mkononi, alitamani sana kuwa na maisha mazuri kama ya wenzake.

Siku moja akiwa anatoka chuo kuelekea nyumbani alikutana kaka mmoja aliyekuwa anaendesha gari aina ya Alteza "Mambo mrembo, unaelekea wapi mamii" Yule kaka alimwita Ritha huku akipunguza mwendo wa gari lake. Ritha alimtizama yule kaka na kusema "Hapana asante, nitapanda tu daladala" Yule kaka akaendelea kusema "Samahani lakini mrembo,nakuomba mara moja kuna jambo nilikuwa nataka nikuulize" Basi Ritha akasogea karibu "Uliza tu hakuna tatizo" Kumbe yule kaka alimwita kwa ukaribu ili ambembeleze apande kwenye gari yake. Haikupita muda Ritha alikubali kupanda kwenye lile gari na waliendelea kuzungumza na kufahamiana.

Yule Kaka alikuwa ni mfanyabiashara, anaitwa Godson.Kutokana na Ritha alikuwa hana simu ya mkononi Godson alimuahidi kumnunulia simu, na kesho yake angempelekea pale chuoni. Baada ya kumfikisha Ritha maeneo ya nyumbani, alimpatia kiasi cha shilingi elfu hamsini "Kiasi hiki kidogo cha pesa kitakusaidia, kwa nauli siku ya kesho, nimefurahi sana kukufamu Ritha, wewe ni mrembo ukinipa nafasi katika moyo wako, nakuahidi utafurahi sana" Ritha huku akiuma vidole vyake kwa aibu akapokea ile pesa na kusema "Asante sana Godson, ila naomba ukanishushe kwa pale mbele hapa Mama akiniona itakuwa balaa" Basi akasogea mbele kidogo na kumshusha.

Ritha alikuwa anatabasamu  huku akizungumza na nafsi yake "Jamani, leo ni siku yangu ya bahati, huyu kaka anaonekana ni mtu mwenye pesa sana, yaani amenipa shilingi elfu hamsini ijapokuwa sijamjibu chochote kuhusu ombi lake, mmmh yaani huko chuoni watanikoma, kwanza hii pesa niifiche vizuri, nikienda Mwenge nanunua viwalo kwa kwenda mbele" Siku hiyo Ritha alikuwa  na furaha sana. Kesho yake kama kawaida alikwenda chuoni, alipotoka tu alimkuta Godson anamsubiri.

 Moja kwa moja  walisalimiana na alimpakia katika gari lake wakiwa ndani ya gari Godson alimpa Ritha simu nzuri ya mkononi aina ya samsung galaxy. Ritha kwa furaha alimkumbatia Godson huku akimbusu na kusema "Asante sana, jamani nimefurahi sana, kweli nimeamini unanipenda Godson" Huku akicheka Godson akasema "Nimekupenda sana Ritha, ukiwa na mimi kila kitu unachokitaka utakipata nipo kwaajili yako".Na huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa mahusiano ya kimapenzi kati ya Ritha na Godson.

Maisha ya Ritha yalibadilika, kwani alianza kuvaa nguo za gharama na alikuwa hapandi daladala tena sasa alikuwa akijakuchukuliwa na kupelekwa chuo kila siku. Na hata wazazi wake walipokuwa wakimuuliza na kumkanya alikuwa awasikilizi aliwadharau na kuona Godson pekee ndiyo wa muhimu katika maisha yake. Aliishi maisha ya starehe sana na kuwadharau watu wengine bila ya kujali chochote. Hata marafiki zake walikuwa wakimshangaa "Mmmh ama kweli watu wanabadilika, sikuhizi Ritha anaringa sana tokea ampate huyo bwana mfanyabiashara" Walikuwa wakizungumza marafiki zake.

Baada ya miezi sita Ritha alipata ujauzito na kuamua kumwambia Godson ambaye alimwambia asijali atamlea vizuri.Basi akawa na kiburi kuwa ataolewa na Godson.Baada ya siku mbili tatu Ritha akiwa hana hili wala lile,  mara alipita muuzaji wa magazeti na moja kati ya yale magazeti ukurasa wa mbele kulikuwa na picha ya Godson na habari ikisema "Mfanyabiashara jambazi asotwa rumande" Ritha hakuamini alichokiona akasogea karibu na kununua lile gazeti kisha kusoma kwa umakini. Ni kweli habari ile ilimuhusisha Godson kutokana na kosa la ujambazi.

 Akiwa anaendelea kusoma ile habari akagundua kuwa Godson alikuwa na mke na watoto watatu. "Mungu wangu, inamaana Godson ni jambazi, na tena kumbe alikuwa na mke? Mama yangu nimekwisha.Nitafanya nini mimi na nina mimba ya miezi minne sasa na nyumbani lazima nitafukuzwa najuta mimi TAMAA IMENIPONZA. Alikuwa anaongea mwenyewe kama mtu aliyechanganyikiwa.

 Baada ya mwezi  mmoja kupita hali ilizidi kuwa mbaya kwani mawasiliano na Godson hayakuwepo tena. Na sasa aliwaomba msamaha wazazi wake na bila hiana wazazi walimsamehe.Hivyo walimlea hadi alipojifungua salama mtoto wa kiume. Na maisha ya Godson haikuelewweka yaliishia wapi kwani watu wengine walikuwa wanasema kuwa baada ya kuachiwa huru alihamia nchi nyingine pamoja na familia yake.

...YALAITI NINGELIJUA.....



                                                                                               Nilijaribu kumuita lakini hakuniitikia na hata nilipomsogelea aliendelea kutembea bila ya kusimama. Nilijisikia vibaya sana, kwani nilijiona nimedharaulika. Hata watu waliokuwepo karibu walinitizama kwa nyuso za kuonyesha kuwa wananionea huruma. Nilibaki nikizungumza na nafsi yangu. "Hivi ni kweli Lema anaondoka na kuniacha, hapana siwezi kuamini nilimuamini kwa moyo wangu wote". 
Nilibaki nalia huku nikijisemea na moyo wangu "Ama kweli dunia hadaa, ulimwengu shujaa na asiyesikia la mkuu huvunjika mguu. Leo hii naumbuka kwa yote haya yaliyotokea katika maisha yangu, lakini mbona sijui kosa langu, inamaana ni kweli amenibadilikia kwa kiasi hiki. Lakini nakumbuka watu wengi walinikanya kuhusu tabia ya Lema lakini mimi nilikuwa nafanya mambo yangu kwa siri sana. 
Tizama sasa nabaki naumia na kuteseka peke yangu. Maisha yangu yote nilimuamini mwanaume huyu. Ndugu, jamaa na marafiki walinikanya lakini nilihisi labda wananione wivu leo hii najuta kwani siamini kama kweli Lema amenitendea yote haya. Alikuwa amejiinamia chini Salima huku akilia kwa uchungu. Maumivu makali moyoni mwangu eeh Mungu nisaidie.

Sikuamini kilichotokea, lakini ndiyo hali halisi maji yamekwisha mwagika hayazoleki tena.Nikiwa naendelea kuwaza alikuja rafiki yangu kipenzi Anna na kunishika begani huku akisema "Pole sana Salima muombe sana Mungu atakusaidia" Wakati Anna akiniliwaza machozi yaliendelea kunibubujika kwa wingi katika paji la uso wangu. Baadaye nilinyanyuka na kuelekea nyumbani taratibu.Maisha yangu yamekuwa na mtihani mkubwa sana. Baada ya kukutana na Lema mwanaume ambaye nilifikiri atakuwa ndiye chaguo la maisha yangu. Lakini haikuwa hivyo nikikumbuka siku ya kwanza tulikutana nikiwa natoka kazini kuelekea nyumbani nikiwa naendesha gari langu aina ya Rav 4. 
Katika maeneo ya Posta jioni usafiri huwa ni wa shida sana.Katika kituo cha daladala kulikuwa na watu wengi wakisubiri usafiri huo.Mimi nikiwa katika foleni kaka mmoja alikuja karibu na gari yangu na kunisemesha "Samahani dada, unaweza kunisaidia lifti" Nilimtizama yule kaka na kusema "Mimi naelekea Kijitonyama, kwani wewe unaenda wapi?" Akanijibu kwa haraka "Naelekea hukohuko dada yangu naomba unisaidie" Haikuwa kawaida yangu kuwapa lifti watu barabarani hususani mtu nisiyemfahamu lakini niliamua kumsaidia huyu kaka.


Siku moja Lema aliniomba tutoke pamoja kwani kuna jambo angependa kunieleza. Siku hiyo ilikuwa ni siku ya furaha kwangu kwani nilikuwa napenda sana kuwa karibu na Lema wakati wote.Tukiwa tumeketi maeneo ya Makumbusho, Lema hakusita kuniambia juu ya hisia zake "Nikikutizama Salima wewe ni mwanamke mrembo sana, wakati mwingine najiona kama sistahili kuwa karibu yako lakini siku zinavyozidi kwenda, upole na ukarimu wako unanifanya nikupende zaidi. 
Natamani ungekuwa mpenzi wangu yaani uwe furaha ya milele katika maisha yangu, nakupenda sana Salima." Huku akiwa ananitizama alisema Lema.Mimi nilikuwa nimejiinamia kwa aibu "Asante Lema, hata wewe ni kijana mzuri sana.Ila siamini kama hauna mwanamke unayempenda." Lema alitabasamu nakusema "Nulijua utaniuliza hivyo, ni kweli nishawahi kuwa mpenzi lakini tulitenganana ni muda mrefu sasa niko peke yangu. Lakini moyo wangu umekutana na mwanamke mwenye kila sifa nilizokuwa nazihitaji ni wewe Salima naomba unipe nafasi katika moyo wako" Moyoni mwangu nilikuwa nikiwaza kwa kiasi gani nilikuwa natamani Lema awe mpenzi wangu na sasa hatimaye ndoto zangu zimekamilika.

Tulizungumza na baadaye nilimwambia Lema anipe muda nitafakari juu ya ombi lake. Baada ya wiki moja hatimaye tulifungua ukurasa mpya wa mapenzi motomoto. Nilimpenda sana Lema kwa moyo wangu wote. Nikiwa katika mahusiano ya kimapenzi na Lema sikuwahi kuwaambia marafiki wala ndugu zangu. Mapenzi haya niliyafanya siri kwa imani kwamba ipo siku Lema atakuja kujitambulisha nyumbani. Baada ya miezi mitatu, siku moja nilikutana na rafiki yangu mmoja anaitwa Sindy tulisalimiana "Jamani Salima nilikuwa nakutafuta sana, vipi mbona simu yako nikikupigia sikupati hewani au umebadili namba".
 Ni kweli nilikuwa nimebadilisha namba ya simu akaendelea kuzungumza "Unajua nilikuwa nakutafuta nikupe taarifa za msiba wa Belinda, si unajua alikuwa anaumwa sana" Nilishangaa kwani Belinda nilikuwa nikimfahamu "Maskini jamani, sikuwa na taarifa daah " Sindy akasema "Ndiyo hivyo ndugu yangu, huyu Lema atawamaliza wadada wa mjini" Nilihisi labda nilikuwa sijamsikia vizuri na kusema "Eti umesema Lema! Atawamaliza wadada wa mjini?".
 Niliuliza kwa shauku lakutaka kujua ni Lema yupi "Inamaana wewe humjui Lema kijana mmoja mtanashati. Anaishi karibu na maeneo ya pale kwenu yaani yule kijana anajijua kabisa ni muathirika lakini huwa anawaambukiza wadada wa mjini kwa makusudi" Nilihisi kuishiwa nguvu lakini ilinibidi nijikaze ili Sindy asielewe chochote.

Baada ya Sindy kuondoka, nilijikuta machozi yakinitoka na kuwaza sasa nitafanyaje kumbe Lema alikuwa na tabia chafu zilizojificha. Akili ikanituma niende kupima afya yangu kwanza. Maskini sintokaa nisahau ni kweli nilikuwa nimeathirika na moja kwa moja nilimjua aliyeniambukiza virusi vya UKIMWI na sasa nilirudi nyumbani huku nikiwa nimekata tamaa kabisa. Nilipofika nikiwa nmeketi kibarazani huku natafakari ghafla alipita Lema akiwa ameongozana na mwanamke nilimwita lakini hakuniitikia na hata niliposogea karibu alijifanya kuwa hanijui kabisa. Moyoni mwangu nilibaki naumia na kujuta kumuamini Lema kijana ambaye ni tapeli wa mapenzi na sasa ameniacha na maumivu ya milele.
Usimuamini mtu kwa haraka fahamu kuwa Majuto ni Mjukuu. na pia kumbuka usiache mbachao kwa msala upitao.


SIYO KILA UNACHOKIWAZA MOYONI MWAKO KITATOKEA KAMA UNAVYOTAKA.

 
                                                                                              Kijana mmoja alitokea kumpenda sana dada mmoja ijapokuwa dada huyo alikuwa akimtolea nje mara kwa mara lakini kijana hakukata tamaa, akiendelea kurusha ndoano huku akiamini siku moja atafanikiwa.Siku moja dada huyo akiwa yupo nyumbani aliamua kumpigia simu huyu kaka na kumtaka aje nyumbani kwake, yule kijana alifurahi na kuhisi sasa ombi lake limekubaliwa. 


Akiwa nyumbani kwake dada huyo , alikuwa amevalia kanga moja laini, kutokana na hali ya hewa ya joto la Dar es salaam.Kwa upande wa yule kijana alikuwa amefurahi sana na haraka alijiandaa na kuanza safari kuelekea kwa huyu dada, njia ni kaka huyu alikuwa akijiuliza maswali mengi, huku akiwa haamini kama yule dada amemuita nyumbani kwake. Alipofika, alibisha hodi na yuel dada akafungua mlango huku akionyesha tabasamu pana katika paji la uso wake. 



Kaka huyu aliingia ndani huku kijasho kikimteremka mithili ya mtu aliyekuwa anakimbia. Dada huyu alimkaribisha vizuri, yule kaka aliomba maji ya kunywa huku muda wote akimtizama kwa umakini dada huyu mrembo, aliyeumbika kila idara na ile kanga nyepesi aliyovaa ilikuwa ikionyesha umbo zuri la dada huyu ambaye waswahili huwa wanasema, mtoto kajaaliwa (mashalaah) Kaka alikuwa akivuta pumzi kwa haraka haraka, na kusema "Nimefurahi sana, umenikaribisha nyumbani kwako ni pazuri sana." Yule dada alitabasamu na kusema "Asante sana, nimefurahi pia umeitikia wito wangu, samahani kwa usumbufu wangu".
Yule kaka alitabasamu huku akijisogeza sogeza "Hakuna tatizo, usijali kabisa, mimi nipo kwa ajili yako, naimani sasa nina...." Kabla hajamilizia kuongea yule dada alimshika mikono yake miwili huku akimtizama machoni, kwa macho yake malegevu, mithili ya mtu aliyekula kungu "Samahani kaka, mimi nimekuita hapa kuna jambo nataka unishauri, nataka kujua ni zawadi gani nzuri unaweza kumpatia mwanaume unayempenda" Kaka yule alikuwa akitetemeka na kusema "Chochote tu, zawadi ni zawadi, alimradi kuwe na mapenzi ya kweli" Dada yule alitabasamu na kusema "Ni kweli, mapenzi ya kweli ndiyo jambo la msingi, nitampenda maisha yangu yote" Kaka yule akauliza "Utampenda? Nani huyo"
.
 Yule dada alitabasamu tena na kusema "Samahani, rafiki nilikuwa sijakuambia, wiki ijayo nafunga ndoa na mpenzi wangu wa muda mrefu ambaye nampenda sana, na pia nilikuita ili nikupe kadi ya harusi, nitafurahi kukuona, kwani wewe ni rafiki yangu pia" Yule kaka alibaki amepigwa na butwaa, "Ati, nini unaolewa, daaah, jamani, kwahiyo." Alinyanyuka na kuondoka bila ya kuaga huku akimuacha yule dada anamuita ili ampatie kadi bila ya mafanikio

STORI YA KWELI YA AJABU NA YAKUSISIMUA













Kulikuwa na mzee mmoja ambaye alikuwa tajiri sana, Mzee huyu alibahatika kuwa na binti mmoja na ambaye alimpenda sana na hata
kumwandika kuwa mrithi wa mali zake zote pindi mzee atakapoiaga dunia.

Mzee huyu alimiliki biashara kubwa sana sana na zenye kuingiza kipato kikubwa na aliogopeka
sana sana katika eneo hilo hasa kwa kwa utajiri wake na ukatili wake pia.

Siku moja mzee huyo alipata taarifa kuwa mtoto wake wa pekee alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na kijana mmoja ambaye anatoka
katika familia isiyojiweza na tena ya kimaskini sana,na wazai wake walikuwa wakifanya kazi katika
moja ya mashamba ya tajiri huyo.

Yule tajiri alijawa na hasira na kuona kama ilikuwa ni fedhea kubwa sana kwa familia yake
na akamuita binti yake na alipomuuliza binti yake alikubalia, mzee kwa hasira akawafukuza
wale wazee na kuahidi kutoa fedha nono kwa polisi yeyote atakaye mtia mbaroni kijana Yule.

Basi kijana Yule ikabidi amfuate binti na kumwambia hali halisi na kuwa sasa wazazi wake wako katika hali mbaya na yeye anasakwa hivyo
ni vyema wakiachana maana anaona Maisha yake yapo hatarini pamoja na familia yake.

Binti Yule akawa akiiba fedha na kuwapelekea wazee wale ili wajikimu na baadae akamshauri
Yule kijana kuwa wakimbie waende mbali wakajifiche na kuanza maisha yao wakiwa kama mme na mke. 

Baada ya mabishano ya siku
kadhaa Yule kijana akakubali na binti akachukua fedha nyingi za kuweza kuanza maisha popote
pale watakapoamua kuishi.

Yule tajiri alipatwa na butwaa na hakuamini kama binti yake kakimbia, akaamua kuwachukua
wazazi wa yule kijana na kuwafunga bila mafanikio na kuamua kuwaachia huru. 

Mkewe na yule tajiri aliendelee kuhuzunika na kunung’unika kwa muda wote mpaka mmewe
akaamua kutoa tangazo kwenye magazeti ya nchi ile na kusema amemsamehe mwanae hivyo
arudi tu na ameafikiana nao kuwa waoane. Hivyo warudi kwa ajili ya harusi.

Taarifa zikamfikia yule kijana akiwa na mpenzi wake yule mtoto wa tajiri, kwa pamoja wakaamua kurudi na wakapokelewa na yule
mzee ambaye akawaambia kuwa watafunga harusi mapema wiki itakayofuata na gharama
zote zitakuwa zake na yule kijana
atashirikiana na yule binti katika kusimamia mali za yule mzee.

Siku tatu baadae wakaamua waende kuandaa suti na shela kwa ajili ya harusi, waingia kwenye
duka la nguo za harusi binti alivyaa shela ikawa imemkaa safi sana na yule kijana naye suti ilimfaya aonekanye maridadi sana,akaamua
kabla ya kuvua ile nguo avuko barabara aende akanunue ice cream maana binti Yule alikuwa
anapenda sana kula ice cream.

Wakati kanunua ile ice cream na anavuka barabara gari likamgonga yule kijana na yule binti baada ya kuona vile alimkimbilia na
alipofika pale damu iliruka na kutengeneza doa kwenye ile shela, wakamchukua na kwenda nyumbani ambako baadae mazishi yalifanyika.

Baada ya mazishi binti Yule aliendelea kuhuzunika na hakutoka ndani kabisa.

Siku moja baada ya miezi kadhaa kupita usiku akiwa kalala alimtokea bibi mmoja na kumwambia katika ile shela kuna doa hivyo
anatakiwa alifuo litoke au balaa litamtokea. 

Yule binti kweli asubuhi aliamka na kwenda kuitazama ile shela na kukuta ina doa, akafua sana mpaka doa akaona limeoptea. Lakini
alipolala tena Yule bibi akamtokea tena na kumwambia lile doa halijatakata hivyo afue tena
au balaa itaikumba familia yake.

Siku ya pili akaamka na kufua lakini kila alipofua yule bibi alimtokea na kumwambia vile viele,yule
binti akaona sasa kachoka ni vyema amshirikishe mama yake.

Mama yake akashangaa sana kwani
naye aliota ndoto kama ile ile na alikumwa akiogopa kuwashirikisha. Mama na mtoto wakanya siri na kulifua tena lile shela na hata
baada ya kulifua yule bibi aliwatokea tena na kuwaambia kuwa bado doa lipo.

Mmmh kazi ikawa ngumu ikabidi wamshirikishe baba, baba naye kumbe wamekuwa akitokewa na
yule bibi na akawa anona sio vyema kuwashirikisha wanafamilia.

Basi baba akawaamuru waichukue ile shelana kwenda kuifukia. 

Baada ya kuifukia Yule bibi aliwatokea na kipindi hiki alikuwa mkali zaidi na kuwaambia wana siku mbili tuu za kulifukua lile shela na kulifua mpaka doa litakate la sivyo kuna jambo kubwa litawatokea .

Familia nzima walilifua kwa ushirikiano na wakakubaliana kuwa sasa limetakata na wakalianika na kulipiga pasi baada ya kukauka na uliweka sandukuni.
Usiku wakiwa wamelala.waliambia wameshindwa.

Basi familia siku ya pili walikutana na kusimuliana wote wakaonyesha
kuota ndoto sawa. Siku ya pili wote wakaenda kazini na kumwacha yule binti aiwa nyumbani peke yake.

Akiwa kaka peke yake na huku akisubiri mwisho wake huku akilia kwa uchungu na kumkumbuka
mchumba wake yule kijana,mara mlango ukagongwa na baada ya kumkaribisha binti yule alistaajabu kuona ni yule yule bibi mzee ambaye amekuwa akiwatokea usiku. Lakini mara hii alikuwa kashika kopo dogo mkononi na
kumpa yule binti kasha akaondoka zake.

Je unafikiri Yule bibi kizee alimpa kopo la nini?

Jibu ni kuwa alimpa kopo la sabuni ya unga aina
ya omo ambalo hutoa madoa kwa uhakika

Ha ha ha ha ha ha ha ha ni janga sana.
Kama ulisoma huku ukifikiria uchawi shindwaaaaaa